Home » » Wenje amvaa Meya

Wenje amvaa Meya

MBUNGE wa Nyamagana jijini Mwanza, Ezekiel Wenje (CHADEMA), amemshambulia Meya wa jiji hilo, Stanslaus Mabula (CCM), akimuita ni mzigo aliyesababisha jiji kuwa na ukata mkubwa wa fedha za maendeleo.
Alisema pamoja na jiji kukumbwa na ukata huo, Mabula ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Mkolani, amesababisha jiji hilo kuwa chafu na kwamba amekuwa akiwakashifu na kuwabeza wafanyabiashara wadogo (Machinga).
Wenje alitoa shutuma hizo juzi wakati akihutubia mamia ya wakazi wa Jiji la Mwanza, katika mkutano wa hadhara wa Operesheni M4C Pamoja Daima, uliofanyika viwanja vya Furahisha.
Huku akimuita Mabula Meya wa ‘Kichina’, Wenje alisema kwa sasa halmashauri hiyo imekumbwa na tatizo kubwa la ukosefu wa fedha, huku viongozi wake wakilalamikia hali hiyo.
“Huyu Meya wa Kichina, analalamika eti jiji halina hela. Wakati anatakiwa na miwani yake afanye kazi kwa ubunifu ili vyanzo vya mapato viongezeke, amebaki akilialia.
“Wakati CHADEMA ilipoongoza jiji hilo kabla ya kuhujumiwa na CCM, jiji lilikuwa na fedha nyingi kutokana na vyanzo vyake, na lilikuwa safi nchi nzima,” alisema.
Kwa mujibu wa Wenje, kwa sasa Mabula analalamika kuwa jiji ni chafu kwa sababu mbunge aliruhusu kuwepo machinga mjini.
“Kwani machinga ni uchafu? Mama ntilie ni uchafu?” alihoji Wenje kisha kushangiliwa.
Akizungumzia ugumu wa maisha unaowakabili wananchi kwa sasa, alisema Bunge lijalo wabunge wa CHADEMA watapambana bungeni kuhakikisha bei ya umeme inashuka kuliko ilivyo sasa.
Kwa mujibu wa Wenje, Watanzania wategemee kuona harakati za wabunge wa CHADEMA wakipigania maendeleo ya wananchi, na kwamba wapo tayari kupigwa ngwara zaidi ya ilivyotokea kwa Mbunge wa Mbeya mjini, Joseph Mbilinyi ‘Sugu’.
“Bei ya umeme imepanda, chumvi, sukari, sabuni na kila kitu. Wamepitisha bei ya umeme sisi tukiwa nje ya Bunge kwenye likizo. Tunasema tukirudi kwenye Bunge haki ya mama mpaka kieleweke, kama mlivyoona wakimnyanyua Sugu, tupo tayari watunyanyue mara 10 ya Sugu,” alisema.
Mbunge wa Ilemela, Highness Kiwia (CHADEMA), alimtuhumu Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Injinia Evarist Ndikilo, kwa madai kwamba amekuwa akikwamisha maendeleo ya wananchi wa Ilemela.
Kiwia alieleza kwamba kiongozi huyo amekuwa chanzo kikubwa cha kukwamisha maendeleo ya wananchi na alimtaka kubadilika mara moja.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Mwanza Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa