Home » » Dk. Chegeni aishukia kampuni ya madini

Dk. Chegeni aishukia kampuni ya madini

MJUMBE wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC), Dk. Raphael Chegeni, ameitaka kampuni ya uchimbaji madini katika mgodi wa Ngasamo wilayani Busega, Simiyu kufuata sheria za nchi kwa kuwalipa fidia wananchi wanaopisha mgodi huo.
Dk. Chegeni alitoa kauli hiyo juzi wakati alipokuwa akijibu maswali ya baadhi ya wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika Kata ya Ngasamo, ikiwa ni maadhimisho ya miaka 37 ya kuzaliwa kwa CCM.
Baadhi ya wananchi walihoji sababu za wao kuondolewa katika maeneo yao bila kulipwa fidia, jambo lililoonekana kumshitua Dk. Chegeni.
Alisema mwekezaji yeyote lazima ahakikishe anafuata taratibu na sheria za nchi katika utekelezaji wa majukumu yake.
“Nimesikitika kusikia hampewi haki zenu. Nataka kila mtu anayetakiwa apishe eneo hilo alipwe fidia yake. Na mwekezaji naye lazima afuate na kuzingatia sheria katika hili,” alisisitiza.
Kuhusu utekelezwaji wa miradi ya umeme vijijini na majisafi ya kunywa, alisema wakati akiwa mbunge wa Busega, alipigania miradi hiyo na mingineyo, jambo ambalo serikali iliiweka kwenye mipango ya utekelezwaji, na sasa imeshaanza kutekelezwa.
Alisema kwa sasa umeme wa vijijini (REA), umeshaanza kusambazwa katika baadhi ya vijiji vya jimbo hilo, huku mradi mkubwa wa maji ya Ziwa Victoria ukiwa katika utekelezaji, na tenki kubwa la maji litajengwa maeneo ya Ngasamo.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Mwanza Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa