Home » » Jaji Sumari awakoromea maofisa upelelezi

Jaji Sumari awakoromea maofisa upelelezi

JAJI Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza, Aishieri Sumari, amesema kesi nyingi za makosa ya jinai zimekuwa zikichelewa kutolewa uamuzi kutokana na baadhi ya maofisa upelelezi kutokuwa na utaalamu wa kutosha.
Jaji Sumari alitoa kauli hiyo jijini Mwanza jana  kwenye maadhimisho ya Siku ya Sheria yaliyofanyika viwanja vya Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza jijini hapa.
Alisema kesi nyingi za makosa ya jinai zimekuwa zikichelewa kutolewa hukumu na hiyo inatokana na kuwepo kwa wapelelezi wasiokuwa na utaalamu wa kutosha.
Alisema ipo haja kwa serikali kuwapiga msasa kwa kuwasomesha zaidi maofisa upelelezi, kwani hakuna sababu ya mtuhumiwa kukaa mahabusu miaka mitano hadi sita bila upelelezi kukamilika.
“Kesi nyingi za jinai zinachelewa kutolewa hukumu kutokana na baadhi ya wapelelezi ni wabovu na wanachelewa kukamilisha kazi zao kwa wakati.
“Naiomba serikali iwapige msasa maofisa upelelezi, ili waweze kwenda na kasi ya utendaji wa majukumu yao. Lazima watu watendewe haki. Upendeleo na uonevu uondolewe  na masilahi kwa watumishi wa mahakama yaboreshwe,” alisisitiza Jaji Sumari.
Aidha, aliiomba serikali pindi inapoanzisha wilaya na mikoa mipya nchini, lazima izingatie uwepo wa majengo ya mahakama katika maeneo husika, ikiwa ni pamoja na kuweka vifaa vya teknolojia ya kisasa, ili kurahisisha utendaji kazi.
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Injinia Evarist Ndikilo, alihimiza mahakama za Mwanza kutafutiwa majengo sehemu nzuri na bora ili mhimili huo uweze kufanya kazi zake kwa uhuru zaidi bila kuingiliwa.
Chanzo;Tanzania Daima 

0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Mwanza Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa