Home » » Wapinga kamati za kata kupewa fedha

Wapinga kamati za kata kupewa fedha

WANANCHI wa Wilaya ya Magu mkoani Mwanza, wamepinga utaratibu wa serikali kupitisha fedha za miradi ya maendeleo kwenye Kamati za Maendeleo ya Kata (WDS), na kusema fedha hizo zinapaswa zipelekwe moja kwa moja katika serikali za vijiji husika.
Walisema mfumo huo ni mbovu, na unachangia kuwepo kwa ufisadi na kushindwa kutekelezwa kwa miradi kama ilivyopangwa katika bajeti ya serikali, hivyo ni vema fedha hizo zikawa zinapelekwa kwenye akaunti za vijiji vilivyopangiwa miradi.
Hayo yameelezwa juzi na washiriki wa mdahalo ulioandaliwa na Shirika la Kutetea Haki za Wanawake na Watoto la TABCO, kupitia mradi wake wa ushirikishwaji wa wananchi katika kupanga bajeti ya serikali ngazi ya vijiji na mitaa, iliyofanyika ukumbi wa Consolata mjini Nyanguge, Magu.
Wakichangia kwenye mdahalo huo uliowashirikisha wananchi kutoka kata tatu za Kitongosima, Nyanguge na Mwamanga wilayani Magu, waliwalalamikia wajumbe wa WDS kwa madai wengi wao hawawaelezi wananchi fedha zilizotolewa na serikali kwa ajili ya maendeleo ndani ya vijiji vyao.
“Miradi mingi wananchi wanaona inajengwa tu. Utaona barabara inatengenezwa au kisima, zahanati bila wananchi kushirikishwa wala kuambiwa hizi hela zimetoka wapi. Hii yote inatokana na kamati za maendeleo ya kata kuwa wasiri sana. Hawasemi wala kusoma mapato na matumizi hawafanyi hivyo,” alisema.
Akizungumza katika mdahalo huo, Mkurugenzi wa TABCO, Keneth Edward, alisema mamlaka zote lazima ziwashirikishe wananchi katika mipango yote ya maendeleo, ikiwemo bajeti za vitongoji, mitaa na serikali za vijiji.
“Sisi TABCO tunahitaji kuona kila mwananchi anashirikishwa katika masuala yote ya kimaendeleo. Wananchi ndio nguzo ya maendeleo, haiwezekani wawekwe kando kwenye mambo muhimu kama haya,” alisema.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Mwanza Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa