Home » » WENJE AONYA MAKANDARASI

WENJE AONYA MAKANDARASI

MBUNGE wa Nyamagana, Ezekiel Wenje (CHADEMA), ametishia kuwachukulia hatua kali makandarasi watakaojenga miradi ya zahanati na wodi ya wazazi, inayotekelezwa na fedha za Mfuko wa Jimbo (CDCF), chini ya kiwango.
Wenje, alitoa onyo hilo juzi alipozungumza na waandishi wa habari, baada ya kutembelea na kukagua ujenzi wa miradi hiyo katika kata tatu za Mahina, Isamilo na Buhongwa jijini hapa.
Alisema katika ziara yake hiyo aliyoongozana na wajumbe wa kamati ya mfuko wa jimbo lake la Nyamagana wakiwemo wataalamu na watendaji wa kata husika, alibaini mradi wa Mahina kuonekana kujengwa chini ya kiwango.
“Mkataba wetu na makandarasi wa miradi yote hii ni kwamba, ikibainika amejenga chini ya kiwango lazima abomoe na aanze kujenga upya kwa gharama zake.
“Wodi ya wazazi Mahina tumeona kuna nyufa na mmomonyoko fulani wa saruji. Sasa nimeagiza wataalamu wafanye ukaguzi, na ikibainika mkandarasi amejenga chini ya kiwango lazima achukuliwe hatua kali. Abomoe na kujenga kwa gharama zake,” alisisitiza Wenje.
Miradi hiyo na gharama zake kwenye mabano ni zahanati ya Isamilo (sh mil. 15), wodi ya wazazi Mahina (sh mil. 20), zahanati ya Isebanda Buhongwa (sh mil. 15).
Wenje alieleza kwamba fedha za mfuko wa jimbo lake zitatumika kujenga miradi hiyo kuanzia msingi hadi kwenye linta, na baada ya hapo Halmashauri ya Jiji la Mwanza itamalizia hatua iliyobaki.
“Mfuko wa Jimbo la Nyamagana tunapokea sh mil. 42 kwa mwaka, na fedha hizi zote tunazielekeza kwenye miradi ya wananchi wetu. Malengo yetu ni kupeleka maendeleo,” alisema.
 Chanzo:Tanzania Daima

0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Mwanza Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa