SERIKALI
kupitia Wizara ya Maji, imeanza utekelezaji wa mradi mkubwa wa maji
safi na maji taka katika miji ya halmashauri za Geita, Sengerema na
Ukerewe mkoani Mwanza (LVWATSAN II), unaogharimu sh bilioni 48.6.
Hayo yamebainishwa juzi na Naibu Waziri wa Maji, Binilith Mahenge,
wakati akikabidhi magari matano ya majitaka, matrekta na tela zake 8,
pamoja na makontena 104 ya kuhifadhia taka ngumu kwa halmashauri hizo
tatu.
Waziri Mahenge alisema kwamba, mradi huo umetekelezwa kwa ushirikiano
baina ya Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) inayochangia dola milioni
25.8 huku Serikali ya Tanzania ikichangia dola milioni 4.6.
Alisema mradi huo ambao pia unatekelezwa kwa miji mitatu kwa kila
nchi tano mwanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (AEC), unatarajiwa
kukamilika ifikapo Desemba mwaka 2015.
Alisema kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema imetengewa dola milioni 14.9, Nansio dola milioni 8.9 na Geita dola milioni 6.6.
Aidha, naibu waziri huyo alitoa onyo kwa wakurugenzi, wenyeviti na
wahandisi wa maji katika wilaya hizo kuhakikisha mradi huo na vifaa
vyake unatekelezwa kwa malengo yaliyokusudiwa.
Naye, mkurugenzi wa mamlaka hiyo, Anthony Sanga, aliweka wazi idadi
ya vifaa vilivyotolewa kwa wilaya hizo tatu, ambapo Geita ilipata
matrekta na tela zake tatu, magari ya maji taka mawili na makontena ya
taka ngumu 40.
Nyingine ni Sengerema magari mawili, matrekta na tela zake tatu,
makontena 37 ya kutunzia taka ngumu, ambapo Halmashauri ya Wilaya ya
Ukerewe yenyewe ikipewa gari moja la maji taka, matrekta na tela zake
mbili.
Mkurugenzi Sanga alisema mradi huo utasaidia kutunza mazingira,
uboreshaji wa huduma ya maji safi na taka katika bonde la Ziwa Victoria.
Chanzo;Tanzania Daima
0 comments:
Post a Comment