Tone

Tone
Home » » Watu saba watiwa mbaroni mauaji ya Mabina wa CCM

Watu saba watiwa mbaroni mauaji ya Mabina wa CCM

Aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Mwanza, Marehemu Clement Mabina.
 
Watu saba  wanashikiliwa na Jeshi  la  kwa tuhuma  za mauaji  ya aliyekuwa Mwenyekiti  wa  Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Mwanza, Clement  Mabina (56).
Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo, Valentino  Mlowola, alithibitisha kukamatwa kwa watuhumiwa hao  wakati akizungumza na NIPASHE kwa njia ya simu jana mchana.

“Hadi sasa tunawashikilia watu saba kwa tuhuma  za  kuhusika katika mauaji hayo. Hata hivyo, msako  bado  unaendelea ili kubaini  iwapo kuna watu  wengine  zaidi waliohusika kwenye mauaji  hayo ya kinyama,”  alisisitiza Kamanda Mlowola.

Alisema watuhumiwa hao wote ni wakazi wa Kata ya Kisesa wilayani Magu na kwamba hakuwa tayari kuwataja majina kwa maelezo kuwa ni kuepuka  kuingilia upelelezi.

Mlowola, alisema  taratibu zikikamilika watuhumiwa hao na wengine watakaomatwa watafikishwa mahakamani kujibu mashtaka.
Alisema bunduki inayodaiwa kutumika kumuua mwanakijiji Temeli Malemi ni Shortgun na siyo bastola na kwamba ilikuwa mapema kutoa ufafanuzi kutokana na mazingira  ya tukio hilo huku akikemea wananchi kujichukulia sheria mikononi.

Mabina ambaye alikuwa mwana-CCM maarufu mkoani hapa  na Diwani  wa Kata  ya Kisesa wilayani Magu, aliuawa baada ya kushambuliwa na  wakazi wa kijiji cha Kisesa wakati akiwa katika  kitongoji cha Kinyama juzi  kati ya saa 3 na saa 4 asubuhi kwa kushambuliwa kwa mawe na silaha  nyingine za jadi hadi kufa kutokana na mgogoro wa ardhi uliokuwa ukiendelea baina yake na baadhi ya wakazi wa maeneo ya kijiji hicho.

WATU WAKIMBIA MAKAZI

Katika hatua nyingine, wakazi kadha wakiwamo wanaume na vijana, wanadaiwa kukimbilia mafichoni kukwepa mkono wa sheria na msako mkali wa polisi unaiendelea dhidi ya walioshiriki mauaji hayo  ya kikatili.

Hatua hiyo  inatokana na msako huo ulioanza tangu juzi kuendelea kwa kasi.

Mwandishi wa habari hizi aliyetemlea kijijini hapo  jana asubuhi alishuhudia askari waliovalia sare za polisi  makachero wakiendesha msako huo.

Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi kwenye  eneo la tukio, baadhi ya wananchi wamedai kuwa baadhi ya wanaume na vijana wamekimbia makazi yao tangu juzi ili kukwepa kukamatwa na polisi.
Mabina aliuawa wakati akijaribu kujihami kwa kufyatua risasi hewani baada ya kuzungukwa na watu wengi waliokuwa wamebebea silaha yakiwamo mawe na mapanga.Wakati alikajaribu kujihami kwa kufyatua risasi hewani,  inadaiwa ilimuua Malemi.

MAZISHI KESHO AU ALHAMISI
Wakati huo huo;  Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Magu, Isack Zablon, amesema mwili wa Mabina unatarajiwa kuzikwa kati ya kesho na  keshokutwa nyumbani kwake katika kijiji cha Kisesa.

 “Hapa nilipo ninajiandaa kwenda kwenye kikao cha mazishi, lakini pia bado tunasubiri mtoto wa marehemu ambaye yuko jijini Dar es Salaam awasili,”  alisema.

Mabina alikuwa diwani na Mwenyekiti  wa Halmashauri  ya Wilaya  ya Magu mwaka 2000 -2005.
Mwaka 2007-2012  alikuwa   Mwenyekiti wa CCM  Mkoa wa Mwanza.

Aligombea tena uenyekiti wa mkoa huo  katika uchaguzi wa mwaka 2012 na kubwaga na  Mwenyekiti wa sasa, Anthony Diallo.
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mwanza Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa