Tone

Tone
Home » » TCCIA, WAFANYABIASHARA WATOFAUTIANA MWANZA

TCCIA, WAFANYABIASHARA WATOFAUTIANA MWANZA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
Mvutano mkali umeibuka kati ya Chemba ya Wafanyabiashara, Wenye Viwanda na Kilimo (TCCIA) na viongozi wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Mwanza (JMWM) kwenye kikao na Mkurugenzi wa jiji, Halfa Hida.
Mzozo huo uliibuka muda mfupi kabla ya kuanza kikao cha ndani saa 4:00 jana asubuhi mjini hapa, kati ya wafanyabiashara na mkurugenzi wa jiji, ambaye ilidaiwa aliwaalika TCCIA bila kujua kama wanatofautiana kikatiba na jumuiya hiyo.
Katika kikao hicho, watumishi ya halmashauri hiyo wakishirikiana na mgambo waliwazuia waandishi wa habari kuingia ukumbini kwa madai kuwa hawakuwa wamealikwa.
Hata hivyo, muda mfupi wakati kikao hicho kikiendelea, viongozi wa TCCIA wakiongozana na mwenyekiti wao, Eribariki Mmari walitoka ukumbini wakidai kuwa wana dharura.
Taarifa kutoka ndani ya kikao hicho, zilidai kuwa viongozi wa jumuiya ya wafanyabiashara waligoma kuendelea na kikao wakipinga kuwapo kwa viongozi wa TCCIA, jambo lililosababisha mkurugenzi wa jiji kuwaomba radhi.
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara, Christopher Wambura aliwasilisha malalamiko yao kwa mkurugenzi, ikiwamo kutozwa ushuru mkubwa tofauti na viwango vilivyowekwa.
Aidha, malalamiko mengine ni ongezeko la ushuru wa taka, urasimu unaofanywa na ofisa masoko wa jiji na vitendo vya rushwa vinavyofanywa na watoza ushuru.
Madai mengine ni mkurugenzi wa jiji kugoma kukutana na wafanyabiashara hao wanapomhitaji. Mwananchi iliambiwa kuwa Wambura aliomba viongozi wa TCCIA kutoka kabla ya kuanza kikao hicho akieleza kuwa katiba ya jumuiya yao haiwatambui.
Hata hivyo, wakati kikao hicho kinaendelea, mgomo wa wafanyabiashara uliendelea kama kawaida na maduka mengi hayakufunguliwa.
Juzi, mwenyekiti wa TCCIA wa Mkoa wa Mwanza, Elibariki Mmari alisema siyo sahihi kwa wafanyabiashara kugoma, kwani tayari malalamiko yao yamewasilishwa kwa mkurugenzi wa jiji.
Pamoja na rai hiyo, jana maduka mengi yalikuwa yamefungwa, huku polisi wakiwaonya baadhi ya wafanyabiashara waliokuwa wakiwazuia wenzao kufungua maduka kuwa kufanya hivyo ni kuvunja sheria na hatua kali zitachukuliwa kwa wote.
 Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mwanza Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa