Home » » Viboko waharibifu wateketezwa

Viboko waharibifu wateketezwa

ASKARI wa kikosi cha wanyamapori kwa kushirikiana na wananchi wamefanikiwa kuangamiza viboko wawili ambao walikuwa hatari kwa usalama wa watu pamoja na uharibifu mkubwa wa mazao yanayolimwa pembezoni mwa ziwa Victoria.
Tukio hilo lililovuta umati mkubwa wa wananchi limetokea katika Kata ya Nyakato, Mtaa wa Baruti ndani ya Manispaa ya Musoma ambako walikusanyika kushuudia viboko hao ambao wamekuwa wakiwataabisha kwa muda mrefu.
Wakizungumza na Tanzania Daima, baadhi ya wananchi ambao ni wakulima katika eneo hilo wamesema wanyama hao walikuwa wakiwasumbua kwa muda mrefu kwani wamekuwa wakitoka ndani ya ziwa na kuvuka mita 60 kwenda kuharibu mashamba.
Walisema hali hiyo iliwalazimu watoe taarifa katika ofisi za maliasili na utalii na kuanzisha msako wa kuwaangamiza.
Aidha, wananchi hao wameeleza kuwa kuna baadhi ya wakulima ambao walikwisha amua kutojihusisha na kilimo katika maeneo hayo, lakini wamelishukuru Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na kikosi cha wanyamapori kuwaangamiza wanyama hao ambao wamekuwa kikwazo kikubwa katika shughuli za maendeleo.
Chanzo: Tanzania Daima


0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Mwanza Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa