Home » » MBUNGE CHADEMA ASHINDA KESI

MBUNGE CHADEMA ASHINDA KESI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Wilaya ya Ukerewe, mkoani Mwanza, imemwachia huru mbunge wa Ukerewe, Salvatory Machemli (CHADEMA) baada ya upande wa mashitaka kushindwa  kuthibitisha  kosa la uchochezi lililokuwa likimkabili.
Akisoma hukumu hiyo, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa mahakama hiyo, Faustine Kishenyi, alisema kuwa mahakama inamwachia huru mtuhumiwa kwa vile upande wa Jamhuri haukuweza kuleta ushahidi wa kutosha ambao ungeweza kuishawishi mahakama imwone ametenda kosa la uchochezi.
Katika hukumu hiyo iliyokuwa ikisubiriwa kwa hamu kubwa na wananchi wengi, hakimu Kishenyi alisema Jeshi la Polisi lilishindwa kuwasilisha vielelezo mahakamani kama ilivyokuwa katika hati ya mashitaka.
Pamoja na kukosekana kwa vielelezo, upande wa mashitaka pia ulishindwa kuwasilisha kanda (CD) inayodaiwa kurekodiwa wakati  mshitakiwa akitenda kosa  hilo.
Badala yake ni askari polisi watatu waliojitokeza mahakamani kutoa ushahidi dhidi ya mshitakiwa.
Alisema kutokana na Jamhuri kushindwa kuthibitisha uwepo wa kosa la uchochezi, mahakama hiyo imejiridhisha kwamba mshitakiwa hakutenda kosa hilo na inamwachia huru.
Awali ilidaiwa na mwendesha mashitaka wa  polisi,  Inspekta   Samwel  Onyango kuwa  Machemli  (39)  alitoa maneno ya uchochezi  Oktoba 23, 2011 wakati alipohutubia mkutano wa hadhara katika Kijiji cha Nyamanga Ukara.
Katika  kesi hiyo  namba  19, ilidaiwa na upande wa mashitaka kwamba mbunge huyo kwa makusudi  aliwachochea  wananchi  akiwataka kuhakikisha wanapambana na polisi na hata kuwashambulia pale watakapokwenda katika maeneo yao kukamata wahalifu.
Akizungumza mara tu baada ya kutolewa kwa hukumu hiyo, Machemli alidai kuridhika na uamuzi wa mahakama kwa sababu ni wa haki.
“Nimefurahi sana na ninajisikia vizuri kwa sababu kwanza ni kesi iliyokuwa ikisubiriwa kwa hamu na makundi mengi ya watu. Lakini pia imechukua muda mrefu na imekuwa ikinisumbua kwa wakati wote,”alisema.
 Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Mwanza Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa