Home » » Watanzania watakiwa kuwekeza EAC

Watanzania watakiwa kuwekeza EAC

WATANZANIA wakiwamo wafanyabiashara wa viwanda, kilimo na elimu, wametakiwa kujizatiti katika suala la uwekezaji kwenye Soko la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), badala ya fursa hiyo kuwaachia raia wa kigeni.
Kauli hiyo imetolewa mjini hapa juzi na Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Injinia Evarist Ndikilo kwenye ufunguzi wa maonesho ya nane ya biashara ya kimataifa, katika viwanja vya Nyamagana.
Alisema tayari Soko la Afrika Mashariki limeshaanza kufanyakazi, hivyo ni vema Watanzania wakachangamkia fursa hiyo, kwa kuzalisha bidhaa zenye ubora ili kuliteka soko hilo.
Kwa mujibu wa Mkuu huyo wa Mkoa wa Mwanza, uzalishaji wa bidhaa zenye viwango vya kimataifa, ndilo jambo muhimu linalotakiwa katika suala zima la ushindani.
“Tunapokuwa katika maonesho haya ya biashara ya kimataifa, msisitizo wa serikali kwa Watanzania ni kuona wanachangamkia fursa ya Soko la Jumuiya ya Afrika Mashariki.
“Soko hili tayari limeshaanza kufanya kazi, kwa hiyo tusije tukawa watazamaji kwa kuwaachia raia wa kigeni katika biashara hii. Watanzania tuwekezeni na kutangaza bidhaa zetu zenye viwango,” alisisitiza RC Ndikilo.
Awali, Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyabiashara wenye Viwanda, Kilimo na Biashara (TCCIA), Mkoa wa Mwanza, Elibariki Mmari, alisema maonyesho hayo yanazishirikisha nchi zote za Afrika Mashariki, China, Singapore na Misri.
Aliiomba serikali kuangalia uwezekano wa kuondoa vikwazo mbalimbali katika maeneo ya mipakani, kwani kufanya hivyo itarahisisha watu wengi kushiriki maonesho kama hayo.
Mmoja wa washiriki wa maonesho hayo, ambaye pia ni Mkurugenzi wa Beijing China Shop, Celestin Patrick, aliiomba TCCIA kuandaa uwanja mzuri wa maonesho, kwani Uwanja wa Nyamagana hauna hadhi nzuri.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Mwanza Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa