Tone

Tone
Home » » BASI LA ABIRIA LATEKETEA KWA MOTO, ABIRIA TISA WAJERUHIWA, MIZIGO YOTE YATEKETEA

BASI LA ABIRIA LATEKETEA KWA MOTO, ABIRIA TISA WAJERUHIWA, MIZIGO YOTE YATEKETEA





Na John Maduhu, Mwanza

WATU 65, wamenusurika kifo baada ya basi la Kampuni ya Adventure walilokuwa wakisafiria kutoka Mwanza kuelekea Kigoma, kuwaka moto na kuteketea.

Akizungumza na MTANZANIA kwa simu jana, Kamanda wa Polisi, Mkoa wa Kagera, Philiph Kalangi, alisema basi hilo liliteketea moto jana saa nne asubuhi.

Kwa mujibu wa Kamanda Kalangi, tukio hilo lilitokea katika Kijiji cha Nyantakala, kilichopo mpakani mwa Mikoa ya Mwanza na Kagera.

Kamanda Kalangi alisema kuwa, basi hilo lenye namba za usajili T293 BBP, lilikuwa likitoka Mwanza kuelekea mkoani Kigoma na kwamba liliwaka moto baada ya kupata hitilafu katika mfumo wake wa umeme.

Alisema kwamba, baada ya kuanza kuwaka moto, abiria waliokuwamo walianza kutoka nje kwa kutumia mlango wa kawaida pamoja na mlango wa dharura.

“Wakati wa tukio hilo, baadhi yao walipitia madirishani na wengine kwenye milango kwa kuwa kila mmoja alikuwa akitaka kuokoa maisha yake,” alisema Kamanda Kalangi.

Alisema kwamba, pamoja na abiria kufanikiwa kuokoa maisha yao, abiria tisa walijeruhiwa vibaya katika harakati za kujiokoa na wamelazwa katika Hospitali ya Wilaya ya Biharamulo kwa ajili ya matibabu.

"Ndugu mwandishi wa habari, hapa ninapozungumza nawe niko katika eneo la tukio kabisa.

“Hili tukio ni baya sana kwa sababu hakuna mali au mzigo wowote uliookolewa, yaani mizigo yote imeteketea kwa moto pamoja na vitu vingine walivyokuwa navyo abiria kwa sababu walishindwa kushuka navyo kutokana na jinsi tukio lenyewe lilivyotokea.

“Kwa hiyo, baada ya kutoka hapa, natarajia kwenda hospitalini kuwajulia hali majeruhi na nadhani baada ya kumaliza mizunguko hii, nitakuwa katika nafasi nzuri ya kutaja majina yao,” alisema.

Kuhusu abiria wengine walionusurika, alisema walitafutiwa usafiri mwingine na kufanikiwa kuendelea na safari yao kuelekea mkoani Kigoma.

"Abiria wote wametafutiwa usafiri wa kuendelea na safari zao, walichopoteza ni mizigo na vitu vingine, hakuna hata mmoja ambaye hakupata usafiri wa kuelekea alikokuwa akienda,"alisema.

Mwakilishi wa Kampuni ya Adventure jijini Mwanza aliyejitambulisha kwa jina la Ustaadh Juma, alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kusema abiria walionusurika walisafiri na basi jingine na kampuni hiyo lililokuwa likifuatana na basi lililoungua.

Chanzo: Mtanzania

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mwanza Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa