Home » » ILEMELA YAKAMILISHA UJENZI WA MIUNDOMBINU YA ELIMU.

ILEMELA YAKAMILISHA UJENZI WA MIUNDOMBINU YA ELIMU.



Kiasi cha shilingi Bilioni 1.39 kimetumika kukamilisha ujenzi wa miundombinu ya elimu sekondari katika Manispaa ya Ilemela ikiwemo vyumba 59 vya madarasa, matundu 72 ya vyoo na seti ya meza na viti 2750.

Akisoma taarifa ya makabidhiano ya miundombinu hiyo, kwa mkuu wa mkoa wa Mwanza, mkurugenzi wa manispaa ya Ilemela, Bi Ummy Wayayu amemshukuru Rais  Samia kwa fedha hizo na kusema kuwa halmashauri ilipokea fedha kiasi cha shilingi Bilioni 1.41 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya elimu na kutumia shilingi bilioni 1.39  hivyo kufanikiwa kuokoa shilingi milioni 26.64

Kufuatia taarifa hiyo, Mhe Said Mtanda ambae ni Mkuu wa Mkoa wa Mwanza ameupongeza uongozi wa Ilemela kwa namna ambavyo inaendelea kusimamia vizuri  utekelezaji wa miradi ya maendeleo huku akiweka wazi jinsi alivyovutiwa na namna ambavyo Ilemela imeweza kuokoa shilingi Milioni 26.

" Niwapongeze Ilemela kwa usimamizi mzuri wa miradi ya maendeleo, lakini nimevutiwa na taarifa kuwa fedha takribani Shilingi milioni 26 zimeweza kuokolewa"

Ni msimamo wa serikali, kuwa tunapofanya shughuli za usimamizi wa ujenzi wa miradi yoyote sio lazima fedha  iliyopangwa itumike na kuisha yote,tunaweza kuokoa fedhs na kuitumia kwa shughuli zingine ,amesema Mhe Mtanda.

Kwa upande wake Mkuu wa wilaya ya Ilemela  Mhe Mwl Hassan Masala amefafanua kuwa kipindi kama hiki katika miaka ya nyuma jamii ilikuwa ikikimbizana kuchangishana fedha kwa ajili ya ujenzi wa madarasa kinyume na sasa ambapo Serikali ya Rais Samia imeweza kutoa fedha na kujenga madarasa na miundombinu mingine mingi ya elimu hivyo kuwataka wananchi kuendelea kushirikiana katika shughuli za maendeleo.

Nae Mbunge wa Jimbo la Ilemela Mhe Dkt Angeline Mabula amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha nyingi za maendeleo ndani ya jimbo hilo ,akaendelea kusema kuwa Ilemela ya miaka 10 iliyopita sio sawa na Ilemela ya sasa kwani maendeleo yanaonekana

Katika nyakati tofauti wanafunzi wa shule ya sekondari ya Lumala ambapo makabidhiano ya ujenzi wa vyumba vya madarasa yamefanyika, wamemshukuru Rais Samia kwa ambavyo anaendelea kuwajali kwa kuwajengea miundombinu ya elimu kwani inawanufaisha na kuwaboreshea mazingira ya kujifunzia hivyo wakamuahidi kusoma kwa bidii ili wafikie malengo yao.



 



0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Mwanza Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa