NA BENJAMIN MASESE, MWANZA
ASKARI wa Jeshi la Polisi mkoani Mwanza, PC Joel Francis (41)
mwenye namba F.4965 anadaiwa kumpiga Donald Magalata (30) kwa fimbo na
kumsababishia kifo.
Tukio hilo limetokea ikiwa ni wiki moja imepita,baada ya askari
mwingine mkoani hapa Dau Elisha mwenye namba H 852 PC wa kituo cha
Nyamagana kumuua askari mwenzake PC Petro Matiko wenye namba H
5950 kwa risasi na baadaye kujipiga risasi kichwani na kufariki dunia
papo hapo.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana,Kamanda wa
Polisi Mkoa wa Mwanza, Justus Kamugisha alisema tukio hilo lilitokea
Januari mosi, mwaka huu saa moja asubuhi katika kambi ya Polisi
Mabatini.
Alisema siku hiyo, PC Francis alikwenda nyumbani kwake na kumkuta
marehemu ambaye alikuwa rafiki yake wa karibu akiwa amelala.
Alisema baada ya askari huyo kuingia ndani kwake, aligundua pochi
yake ya kutunzia fedha, kadi mbili za benki na kitambulisho cha kazi
vyote vilikuwa havionekani ndipo alipoanza kuhoji.
“Marehemu alikuwa rafiki yake PC Francis, alikuwa akimsaidia kazi
mbalimbali za nyumbani, ingawa marehemu alikuwa akifanya kazi ya ulinzi
hotel ya Mwanza iliyopo katikati ya jiji.
“Sasa mzozo huo, ulisababisha PC Francis kumfunga pingu miguuni
marehemu na kuanza kumpiga ovyo sehemu mbalimbali za mwili kwa kutumia
fimbo kitendo kilichosababisha kupiga kelele kuomba msaada.
“Kelele za kuomba msaada ziliwafanya majirani zake pale kambini
wafike na kumkuta akiwa na hali mbaya na kumchukua hadi Hospitali ya
Rufaa ya Bugando kwa ajili matibabu,”alisema.
Alisema kutokana na kipigo alichopata, marehemu alifariki Januari 2, mwaka huu wakati akipatiwa matibabu.
Alisema tayari jeshi hilo, linamshikilia Pc Francis kwa mahojiano juu
ya tukio hilo na atachukuliwa hatua za kisheria kwa mujibu wa taratibu
wa kijeshi.
Kamanda Kamugisha, alisema anashangazwa na tukio hilo kufanywa na
askari ambaye anapaswa kusimamia sheria na haki za binadamu, huku
akisisitiza kitendo hicho kisichukuliwa kama maadili na maagizo ya jeshi
la polisi, bali ni tabia ya mtu mmoja.
CHANZO GAZETI LA MTANZANIA
0 comments:
Post a Comment