Home » » MWANZA YARINDIMA KWA MABOMU

MWANZA YARINDIMA KWA MABOMU

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399
Wafanyabiashara ndogo ndogo maarufu kama wamachinga wa jijini Mwanza, wakifanya vurugu ya kuziba barabara baada ya mabanda yao yaliyokuwapo eneo la Makoroboi kuvunjwa na mgambo wa Manispaa ya Jiji usiku wa kuamkia jana.Picha/Joel Maduka
Shughuli katika Jiji la Mwanza jana zilisimama kufuatia vurugu kubwa zilizosababishwa na wafanyabiashara ndogo ndogo (wanachinga) wanaofanya shughuli zao katika soko la Makoroboi katikati ya Jiji.
Katika vurugu hizo ambazo mabomu ya kutoa machozi yalitumika kuwatawanya wamachinga, askari kujeruhiwa na watu kadhaa kutiwa mbaroni, zilidumu kwa takribani saa nane.

Polisi wa Kikosi cha Kutuliza ghasia wakitumia mabomu ya machozi, walipita mitaani wakipambana wamachinga hao ambao waliokuwa wakipinga kitendo cha askari wa jiji kubomoa vibanda vyao vya biashara.

Vurugu zilianza saa 12:00 asubuhi baada ya wamachinga kufika eneo la Makoroboi, maarufu kwa maduka ya nguo, na kukuta vibanda vyao vya biashara vikiwa vimevunjwa.

Kuona hali hiyo walivamia msikiti ulio jirani na eneo hilo na kutaka kuuchoma moto kabla polisi wa kutuliza ghasia hawajafika ka kurusha mabomu ya machozi kuwatawanya.

Maduka na masoko katikati ya jiji la Mwanza vilifungwa kwa siku nzima jana wakati polisi wakipambana nao wakipita mtaa hadi mtaa wakifanya vurugu.

Barabara za kuelekea katikati ya Jiji pia zilifungwa na wamachinga baada ya kuweka mawe, magogo na matairi ili kuzuia mabasi ya abiria kuingia katikati ya jiji.

Pamoja na  polisi wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) kutumia mabomu kuwatawanya, wamachinga hao hawakujali na waliendelea kupambana na polisi huku wakiwarusha mawe.

Kituo cha mabasi cha Pansiansi katika barabara ya Kenyatta kilifungwa na wamachinga hao huku wakizuia magari ya abiria kutoka au kuingia katika kituo hicho.

Hadi saa nane mchana, polisi walikuwa bado wanapambana naona walisikika wakisema hawatasalimu amri mpaka watakaporudishiwa vibanda vyao na kuruhusiwa kufanya biashara katika eneo hilo.

Polisi waliweka vizuizi katika barabara zote kubwa za katikati ya Jiji ili kuzuia magari na waenda kwa miguu kwa lengo la kujaribu kuwadhibiti wamachinga ambao walikuwa wanajichanganya na wananchi wengine ili kuwapiga chenga polisi.

Mamlaka ya jiji la Mwanza inaendesha operesheni ya kusafisha jiji, ili pamoja na mambo mengine kuhakikisha kuwa wafanyabiashara ndogondogo wanaofanya kazi katika maeneo yasiyostahili wanaondolewa.

Mamlaka ya jiji imetenga maeneo kwa ajili ya wafanyabiashara ndogo ndogo katika maeneo ya Sahara, Pamba Road, Kenyatta na Barabara ya Posta, lakini baadhi yao wamekataa kuhamia huko.

Mwenyekiti wa chama cha Wafanyabiashara ndogo ndogo, Joseph Samuel, alisema wamachinga waliofanya vurugu jana ni wakorofi tu na kwamba hawawakilishi chama chao.

Vurugu hizo zilisababisha kujeruhiwa kwa  askari  mmoja kutoka kikosi cha  Zimamoto  na  Uokoaji.Baadhi ya watu walioshuhudia tukio hilo, walisema vurugu  hizo zilianza  saa 12:00 baada  ya  wamachinga’ kufika katika maeneo yao ya biashara na kubaini  uharibifu mkubwa uliokuwa umefanywa na  mgambo wa jiji ambao pamoja  na mambo mengine, walitumia tingatinga kuvunja meza zao.

Inadaiwa  kwamba mgambo waliendesha operesheni  hiyo tangu alfajiri ya saa 11 kutokana na agizo kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa.Hata  hivyo, baadhi ya watu waliohojiwa na NIPASHE  kuhusiana na vurugu hizo wameonyesha kusikitishwa kwa  madai kuwa  ni ukiukwaji wa dhana ya utawala bora, kwa kuwa wamachinga hawakupewa taarifa mapema ili waondoke kwa hiari yao.

Habari zinasema kuwa mgambo hao waliokuwa wamefuatana na askari polisi na walifunga  barabara za kuingia eneo la Makoroboi, huku wakiwa  na gari maalum la askari wenye mabomu ya machozi ambayo yalifyatuliwa na kuathiri baadhi ya wapitanjia.

Inadaiwa kwamba kutokana na hali hiyo, machinga waliamua kuvamia ghala la jiji  ili kudai  mali zao, kitendo kilichosababisha mgambo wajifungie ndani ya ghala kuogopa mashambulizi.

Baada ya kudhibitiwa, machinga hao walirejea tena Makoroboi na  kuamua kutekeleza kwa moto vipande vya meza  na  mbao zilizokuwa zimeharibiwa  na  mgambo.

Mkaguzi wa Zimamoto  na Uokoaji ambaye  pia ni Mkuu wa kituo jijini hapa, Augostine Magera, alithibitisha kuwapo kwa tukio la kujeruhiwa kwa askari wa  jeshi  hilo, Nelson Byarugaba.

Magera anayekaimu nafasi  ya Mkuu wa Kikosi cha Zimamoto mkoani Mwanza, alisema askari huyo ambaye ni dereva alipigwa jiwe shingoni  na kupata jeraha.

Hata hivyo hali yake inaendelea vizuri baada ya kupatiwa huduma ya kwanza kituoni hapo.Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Nyamagana, Robert Mwinamila, alisema ofisi yake  imesikitishwa  na unyama unaofanywa na  viongozi pamoja na watendaji wa serikali kutokana  na kukiuka  haki  za binadamu  na utawala  bora.

“Mimi  ndiye  nilimpigia  simu mheshimiwa  Wenje( Ezekiel  Wenje- Mbunge  wa  jimbo  la Nyamagana)  kumjulisha  kilichotokea  leo  asubuhi. Kwa ujumla zoezi  hilo halikuwatendea haki  wamachinga  kwa sababu hawajashirikishwa,” alisema Mwinamila.

Alidai kwamba wamachinga  katika eneo la Makoroboi wanafanya biashara kihalali kwa sababu wana kibali kilichotolewa  na aliyekuwa Mkurugenzi  wa Halmashauri  ya Jiji la Mwanza, Wilson  Kabwe. 

Katibu wa  wamachinga, Renatus Kaizirege, alisema kuwa  zoezi  hilo limetekelezwa  kisiasa kutokana  na shinikizo  la Mkuu wa Mkoa na kwamba wanaopaswa  kushughulikia  suala hilo ni wataalamu wa Jiji la Mwanza kwa kushirikiana  na wamachinga na  siyo vinginevyo.

Diwani   wa Kata  ya Nyamagana, Bhiku  Kotecha  alikataa  kuzungumzia  suala  hilo kwa madai kuwa yeye siyo msemaji wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza.

Alipoulizwa  kwa njia  ya simu jana jioni, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza, Danford Kamenya, alisema  alikuwa kwenye  kikao  na kwamba angetoa  ufafanuzi  baadaye; ingawa hata hivyo  baadaye alipotafutwa hakupokea.

Mkuu  wa  Wilaya ya Nyamagana, Baraka  Konisaga, alipotafutwa alisema alikuwa  kwenye  kikao  kwa  ajili kujadiliana  na watendaji  pamoja  na viongozi wengine  na wilaya  na mkoa kuhusiana  na  suala  hilo.

Kamenya alisema operesheni ya kusafisha Jiji ilianza tangu Mei 17, mwaka huu na kuwa wamachinga walishapewa taarifa.

“Tulianza vizuri alfajiri, lakini wamachinga baadaye walifika na kuanza kufanya fujo, alisema Kamenya na kuongeza kuwa hakuna mali zilizoharibiwa kwa kuwa waliochokuwa wakikifanya ni kuondoa uchafu zikiwamo meza.

Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Baraka Konisaga, alipoulizwa, alisema wenye mamlaka ya kuzungumzia suala hilo ni Halmashauri ya Jiji.

12 WATIWA MBARONI
Kaimu Kamanda wa Polisi mkoa wa Mwanza, Christopher Faime, alisema jana kuwa watu 12 wamekamatwa kuhusiana na vurugu hizo.
Faime amewaomba wafanyabiashara ndogo ndogo kutii sheria na mamlaka na kuhamia katika maeneo waliyotengewa.

WENJE AOMBA MWONGOZO
Mbunge wa Nyamagana, Ezekiel Wenje, jana aliomba mwongozo bungeni kutaka Serikali isitishe operesheni ya kuwaondoa wamachinga inayoendelea jijini Mwanza.

“Muda huu ninapoomba mwongozo wako Msheshimiwa Spika, eneo la Makoroboi jijini Mwanza limechafuka, kuna operesheni inaendeshwa ya kuwaondoa wamachinga.

“Hali hii ikiendelea inaweza kusababisha vifo vya watu na upotevu wa mali zao,” alisema.

Alisema suala la wamachinga limemaliza maisha ya watu mwaka 2011 na mwaka 2012 na linapaswa kutafutiwa ufumbuzi makini.

“Suala la Machinga ni la kitaifa, limetokea Mbeya, Dar es Salaam, Iringa na sasa Mwanza,” alisema na kuongeza karibu miji yote.

Alisema maduka yote jijini Mwanza yamefungwa, hakuna biashara inayoendelea na katika maana hiyo serikali itakuwa inakosa mapato na hata wananchi kukosa huduma na mapato pia.

Baada ya kuomba mwongozo huo kwa Spika, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, alisema suala hilo linashughulikiwa.

“Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, ametoka hapa, anaendelea kuchukua, ameenda kuwasiliana na Mwanza ili kujua nini kinaendelea huko.“Amekuja tu kupiga kura hapa, anaendelea na hatua zitachukuliwa,” alisema Lukuvi

Imeandikwa na Juma Ng’oko,  Rose Jacob, Mwanza na John Ngunge, Dodoma.
 
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Mwanza Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa