Home » » MILIONI 206 KUJENGA ZAHANATI KISIWA CHA BEZI

MILIONI 206 KUJENGA ZAHANATI KISIWA CHA BEZI


Serikali imetenga jumla ya kiasi cha shilingi milioni 206 kupitia mpango wa kunusuru kaya masikini (TASAF-OPEC 4) kwa ajili ya ujenzi wa zahanati na nyumba za watumishi katika kisiwa cha Bezi wilayani ilemela ili kutatua kero ya muda mrefu ya ukosefu wa huduma za afya inayowakabili wananchi wa kisiwa hicho

Hayo yamesemwa na mbunge wa jimbo la Ilemela Mhe Dkt Angeline Mabula wakati wa ziara yake katika kata ya Kayenze mtaa wa Iponyabugali yenye lengo la kusikiliza kero za wananchi na kutoa mrejesho wa vikao vya bunge kwa wananchi ambapo amesema kuwa changamoto ya wazazi kujifungulia njiani wakati wa kufuata huduma za afya umbali mrefu na Gharama kuwa kubwa imepata utatuzi baada ya serikali kuweka mpango wa kuboresha huduma za afya katika eneo Hilo

“Serikali ya awamu ya sita chini Dkt Samia Suluhu Hassan imetenga fedha kwa ajili ya nyumba za watumishi mbili kwa moja milioni 103 na zahanati milioni 103, Kikubwa tuendelee kuunga mkono jitihada za serikali”, Alisema

Aidha Mhe Dkt Mabula akawataka wananchi wa kata hiyo kusimamia na kulinda vifaa vya ujenzi wa miundombinu hiyo visiibiwe ili kukamilisha miradi mbalimbali inayotekelezwa ndani ya kata hiyo pamoja na kuwaripoti wabadhirifu wote wa mali za umma watakaojitokeza ili Sheria ichukue mkondo wake

Gabriel Remmy ni msanifu majenzi halmashauri ya manispaa ya Ilemela amefafanua kuwa mradi huo wa zahanati utakuwa na huduma za baba,mama na mtoto , huduma za wagonjwa wa nje pamoja na nyumba moja itakayojumuisha familia mbili huku akiongeza kuwa kinachosubiriwa ni mifumo ya malipo kuanza kufanya kazi ili mradi uweze kutekelezwa

Kwa upande wake diwani wa kata ya Kayenze Mhe Issa Mwalukila Dida mbali na kuishukuru Serikali na mbunge wa jimbo hilo kwa kuchochea utekelezaji wa miradi ya maendeleo akawataka wananchi wa kata yake kuchangia na kushiriki shughuli za maendeleo ili jamii yao iweze kusonga mbele.


Joachim Sylvester ni mwananchi wa mtaa wa Iponyabugali kata ya Kayenze ambapo amempongeza mbunge Dkt Angeline Mabula kwa kufanya ziara katika mtaa wao kusikiliza kero na kuzipatia ufumbuzi akiambatana na wataalam wa halmashauri ya manispaa ya Ilemela pamoja na wakuu wa taasisi zinazofanya kazi zake ndani ya Jimbo la Ilemela ikiwemo TANESCO, TARULA, MWAUWASA na nyingine


 


0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Mwanza Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa