RAIS John Magufuli amesema aliamua kupeleka Muswada wa Marekebisho ya
Sheria Mbalimbali wa Mwaka 2017 kuhusu ya madini bungeni, kwa hati ya
dharura ili kutetea rasilimali za nchi ili ziwanufaishe Watanzania wote.
Dk Magufuli aliyasema hayo jana mjini hapa mkoani Mwanza, wakati
akizindua rasmi mradi mkubwa wa maji wa Nyamazugo uliojengwa kwa gharama
ya Sh bilioni 21 ambao unatarajia kuwanufaisha jumla ya watu 138,000,
ambapo aliwataka wakazi wa Sengerema kuilinda na kuutunza mradi huo.
Aliwashukuru Washirika wa Maendeleo, Benki ya Maendeleo ya Afrika,
Kamisheni ya Bonde la Ziwa kwa nchi za Afrika Mashariki na Wizara ya
Maji na Umwagiliaji kwa kazi kubwa waliyofanya kwa kukamilisha ujenzi wa
mradi huo.
Kuhusu kauli yake ya wanafunzi wanaopata ujauzito shuleni, alisema
uamuzi wake uko palepale na kuonya kuwa mkuu wa shule yoyote
atakayeruhusu msichana aliyepata ujauzito atasimamishwa kazi.
“Tukiijenga principle (kanuni) hii, ya watoto kujifungua na
kurudishwa shuleni, hakuna mtoto wa kike atakayesoma,” alieleza. Alisema
serikali yake haiwezi kuwasomesha wasichana kwa fedha za walipa kodi na
badala yake akayataka mashirika yasiyo ya kiserikali na wanaharakati
wanaopigia debe suala la wanafunzi wajawazito kurudi shule, wafungue
shule zao ili wawasomeshe wanafunzi wanaopata ujauzito.
Kuhusu safari za nje, alisema hadi sasa amekataa mialiko ya safari za
nje ya nchi ipatayo 60, kwani ameona ni vyema kwanza ashughulikie
changamoto za ndani ya nchi. “Hata jana (juzi) ilitakiwa niende
Ethiopia, lakini nimetuma Makamu wa Rais ameenda huko,” alifafanua na
kuongeza kuwa yeye ni Yohana Mbatizaji anayefanya kazi ya kumsafishia
njia Rais ajaye kwa kuondoa uovu katika maeneo mbalimbali nchini.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu Wizara ya Maji na Umwagiliaji, Profesa
Kitila Mkumbo alisema mradi huo uliozinduliwa na Rais Magufuli ni sehemu
ya programu ya uboreshaji wa huduma za maji kwa miji 15 ya nchi za
Afrika Mashariki, ambapo kwa Tanzania programu hiyo imetekelezwa kwa
miji ya Sengerema, Geita, Nansio na Sirari.
CHANZO HABARI LEO
0 comments:
Post a Comment