Tone

Tone
Home » » JPM: MISWADA YA DHARURA NI KWA MASLAHI YA TAIFA

JPM: MISWADA YA DHARURA NI KWA MASLAHI YA TAIFA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Rais John Magufuli
RAIS John Magufuli amesema aliamua kupeleka Muswada wa Marekebisho ya Sheria Mbalimbali wa Mwaka 2017 kuhusu ya madini bungeni, kwa hati ya dharura ili kutetea rasilimali za nchi ili ziwanufaishe Watanzania wote.
Dk Magufuli aliyasema hayo jana mjini hapa mkoani Mwanza, wakati akizindua rasmi mradi mkubwa wa maji wa Nyamazugo uliojengwa kwa gharama ya Sh bilioni 21 ambao unatarajia kuwanufaisha jumla ya watu 138,000, ambapo aliwataka wakazi wa Sengerema kuilinda na kuutunza mradi huo.
Aliwashukuru Washirika wa Maendeleo, Benki ya Maendeleo ya Afrika, Kamisheni ya Bonde la Ziwa kwa nchi za Afrika Mashariki na Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa kazi kubwa waliyofanya kwa kukamilisha ujenzi wa mradi huo.
Kuhusu kauli yake ya wanafunzi wanaopata ujauzito shuleni, alisema uamuzi wake uko palepale na kuonya kuwa mkuu wa shule yoyote atakayeruhusu msichana aliyepata ujauzito atasimamishwa kazi.
“Tukiijenga principle (kanuni) hii, ya watoto kujifungua na kurudishwa shuleni, hakuna mtoto wa kike atakayesoma,” alieleza. Alisema serikali yake haiwezi kuwasomesha wasichana kwa fedha za walipa kodi na badala yake akayataka mashirika yasiyo ya kiserikali na wanaharakati wanaopigia debe suala la wanafunzi wajawazito kurudi shule, wafungue shule zao ili wawasomeshe wanafunzi wanaopata ujauzito.
Kuhusu safari za nje, alisema hadi sasa amekataa mialiko ya safari za nje ya nchi ipatayo 60, kwani ameona ni vyema kwanza ashughulikie changamoto za ndani ya nchi. “Hata jana (juzi) ilitakiwa niende Ethiopia, lakini nimetuma Makamu wa Rais ameenda huko,” alifafanua na kuongeza kuwa yeye ni Yohana Mbatizaji anayefanya kazi ya kumsafishia njia Rais ajaye kwa kuondoa uovu katika maeneo mbalimbali nchini.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu Wizara ya Maji na Umwagiliaji, Profesa Kitila Mkumbo alisema mradi huo uliozinduliwa na Rais Magufuli ni sehemu ya programu ya uboreshaji wa huduma za maji kwa miji 15 ya nchi za Afrika Mashariki, ambapo kwa Tanzania programu hiyo imetekelezwa kwa miji ya Sengerema, Geita, Nansio na Sirari.

CHANZO HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mwanza Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa