Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
ZAIDI ya walimu 50 kutoka shule mbalimbali za msingi na sekondari
katika Halmashauri ya Manispaa ya Nyamagana mkoani hapa, jana
waliandamana hadi ofisi za mkurugenzi wa halmashauri kushinikiza kulipwa
mshahara wa mwezi uliopita.
Mbali na kudai mshahara, walimu hao pia wanataka kulipwa fedha walizotumia kwa ajili ya nauli wakati wa kuripoti kazini.
Hii ni mara ya pili walimu hao kuandamana, kwani Mei 6 mwaka huu
waliandamana wakitaka walipwe madai yao na kutishia kutoingia
madarasani.
Tanzania Daima ilishuhudia walimu hao wakiwa wamekusanyika nje ya
ofisi za halmashauri ya jiji, wakisubiri kukutana na mkurugenzi,
Halifa Hida, ambaye inadaiwa awali alikuwa safarini kikazi.
Walimu wanaituhumu ofisi ya halmashauri ya jiji kwa uzembe kwa sababu
wenzao walioajiriwa pamoja katika Manispaa ya Ilemela
wameshalipwa mishahara na madai yao mengine.
Habari zimedai kuwa ni walimu 43 pekee ndio wamelipwa mishahara kati
ya 164 waliopangiwa kufanya kazi katika Halmashauri ya Jiji la Mwanza,
mwanzoni mwa mwaka huu, na kwamba wamekuwa wakielezwa kuwa majina yao
yako wizarani, ambako yalitumwa kabla ya Aprili mwaka huu kwa ajili ya
uhakiki.
Ofisa mmoja wa halmashauri hiyo aliliambia Tanzania Daima kuwa walimu
hao wanadai zaidi ya sh milioni 80, na kwamba awali baada ya kuona
wamecheleweshewa mishahara yao, walitaka wakopeshwe fedha ili waweze
kujikimu wakati wakiendelea kusubiri.
Akizungumza kwa sharti la kutotaja jina, afisa huyo alisema uongozi
wa jiji ulidai hauna fedha, na badala yake ukawatuma kwa
walimu wakuu katika vituo vyao vya
kazi ambao pia walisema hawana fedha za akiba kwa ajili ya kuwakopesha.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza, Hida, hakuwa tayari kuzungumzia jambo hilo licha ya kufuatwa.
Chanzo;Mwananchi