Tone

Tone
Home » » ALAT YARIDHISHWA USIMAMIZI WA MIRADI WILAYANI UKEREWE

ALAT YARIDHISHWA USIMAMIZI WA MIRADI WILAYANI UKEREWE

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

JUMUIYA ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT), Mkoa wa Mwanza imeridhishwa na ubora wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika Wilaya ya Ukerewe na kutaka iwe mfano wa kuigwa na wilaya nyingine nchini.
Pongezi hizo zilitolewa jana baada ya wajumbe wa jumuiya hiyo kutembelea miradi mitano yenye thamani ya sh. milioni 693.5 inayotekelezwa katika maeneo tofauti ya wilaya hiyo.
Makamu Mwenyekiti wa ALAT tawi la Mwanza, Henry Matata alisema mbali na miradi ya majengo ya taasisi tofauti waliyotembelea kuwa katika viwango vya kuridhisha pia barabara zake ni nzuri na zinapitika.
Akionekana kufurahishwa na uwajibikaji wa halmashauri hiyo, Matata ambaye pia ni mwenyekiti wa Halmashauri ya mji wa Ilemela, alisema ALAT imetoa mchango wa sh.milioni. 2.1 kuchangia miradi hiyo.
Kati ya fedha hizo sh. 800,000 zimetolewa kwa kikundi cha Bure Garden kinachojishughulisha na kilimo na usindikaji mazao huku kiasi sawa na hicho zikitolewa kukamilisha jengo la kupumzikia wagonjwa katika Hospitali ya wilaya hiyo na sh. 500,000 zikitolewa kusaidia ujenzi wa jengo la utawala katika sekondari ya Mumbuga.
Hata hivyo, alisema jumuiya hiyo inakabiliwa na changamoto kadhaa ikiwemo baadhi ya halmashauri kushindwa kuwasilisha michango yake kwa wakati sababu inayokwamisha mipango ya jumuiya.
Taarifa iliyotolewa katika kikao hicho inaonyesha hadi kufikia mwaka huu halmashauri sita kati ya saba za mkoa huo zinadaiwa sh. milioni 84.3 ambapo Ilemela inadaiwa sh. milioni 9 , Kwimba sh. milioni 5, Misungwi sh.milioni 19, Sengerema sh.milioni 8.5, Magu sh. milioni. 18.3 na Ukerewe sh. milioni 17.5.
Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Joseph Mkundi, akipokea msaada huo, alisema halmashauri yake ipo makini na itaendelea kusimamia kwa karibu shughuli na miradi yote ya umma ili kuiwezesha jamii kupata huduma bora.
Akifafanua zaidi aliunga mkono utaratibu wa jumuiya hiyo waliojiwekea wa kutembelea miradi na kufanya vikao kwa kila wilaya kwa maelezo kuwa unawezesha wajumbe kujifunza mbinu mbadala za maendeleo na kuongeza wigo wa ufahamu katika kusimamia majukumu yake.

Chanzo:Majira

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mwanza Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa